Friday, March 22, 2024

TANZANIA YAWANOA WANAMIBIA MASUALA YA HALI YA HEWA




 


Namibia: Tarehe 18/03/2024.

Tanzania kupitia Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imewanoa watumishi wa Taasisi ya Hali ya Hewa Namibia kwa kuwapatia mafunzo ya kuhakiki weledi wa wafanyakazi wote wanaofanya kazi za kutoa huduma za hali ya hewa katika viwanja vya ndege. Mafunzo hayo yalifanyika katika ofisi za Hali ya Hewa Namibia kuanzia tarehe 04 hadi tarehe 18/03/2024, Windhoek, Namibia. 

Akizungumza wakati wa kufunga rasmi mafunzo hayo, Balozi wa Tanzania nchini Namibia, Mhe. Caesar Waitara aliishukuru Taasisi ya Hali ya Hewa Namibia kwa kuichagua Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzani kuendesha mafunzo hayo,  pamoja na uwepo wa taasisi nyingi za hali ya hewa barani Afrika. Aidha, alizitaka taasisi zote mbili kuongeza ushirikiano zaidi katika masuala mbalimbali kwa lengo la kunyanyua uchumi na maendeleo ya nchi za Kusini mwa Afrika.

“Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imefanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya hali ya hewa nchini kwetu ikiwa ni pamoja na kufunga miundombinu ya kisasa ya hali ya hewa, mafunzo kwa watumishi kwa kuzingatia vigezo vya kitaifa na kimataifa, na  kuweka mifumo wezeshi ya usambazaji wa taarifa za hali ya hewa kwa urahisi kwa watumiaji wa taarifa hizo, pamoja na kuimarisha mifumo ya uhakiki wa ubora wa huduma (QMS) na weledi wa wafanyakazi”. Alisema Mhe.Waitara. 

Aidha, alieleza kuwa Tanzania ilikuwa miongoni mwa nchi za mwanzoni kabisa kufanikisha kupata cheti cha ubora wa kimatiafa cha “ISO 9001:2015” katika utoaji wa huduma za hali ya hewa katika sekta ya usafiri wa anga. Kupitia mafanikio hayo, Tanzania kuipitia TMA imeweza kuzisaidia nchi zingine kama vile Nigeria, Libya, Saudi Arabia, Maldives na Lesotho katika masuala uanzishaji na utekelezaji wa mifumo ya utoaji huduma bora za hali ya hewa katika viwango vinavyotambulika kimataifa. 

Awali, Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Hali ya Hewa Namibia, Bw. Elias Aiyambo, aliishukuru Serikali yake kwa kukubali maombi ya kufanya mafunzo hayo muhimu kwa nchi, vilevile aliishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kufanikisha mafunzo na kuomba ushirikiano huo uendelee baina ya nchi hizi mbili.  

Akitoa mrejesho wa mafunzo hayo kwa mgeni Rasmi, Mratibu wa mafunzo hayo na Mkurugenzi wa Udhibiti na Usimamizi Ubora wa Huduma za Hali ya Hewa TMA, Dkt. Geofrid Chikojo, alisema wamefanikiwa kutoa elimu kwa wafanyakazi 20 wanaofanya kazi katika viwanja 8 vya ndege pamoja na Makao makuu. Kati ya hao 19 walifanikiwa kufanya majaribio ya weledi ambao 17 waliweza kuthibitisha kuwa na weledi unaotakiwa. Dkt. Chikojo alitoa ushauri kwa Serikali ya Namibia kuwa na mpango wa kuhakikisha mifumo ya uhakiki wa ubora wa huduma na weledi inaendelea kuimarishwa na kuwatumia ipasavyo wafanyakazi waliopata vyeti vya weledi katika mafunzo yaliyofanyika.







Saturday, March 16, 2024

KAMATI YA BUNGE YA KUDUMU YA MIUNDOMBINU YAPONGEZA UWEKEZAJI MKUBWA SEKTA YA HALI YA HEWA










Mwanza; Tarehe 16 Machi, 2024


Kamati ya Kudumu ya Miundombinu ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeipongeza Serikali kwa uwekezaji mkubwa kwenye sekta hali ya hewa nchini wakati wa ziara ya ukaguzi wa miradi inayotekelezwa na TMA ikiwemo rada ya hali ya hewa iliyopo Kiseke, Mwanza, Tarehe 16/3/2024.

Pongezi hizo zilitolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe.Seleman Kakoso (MB) wakati wa majumuisho ya ziara hiyo kwa kuridhishwa na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali kwenye Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania na kupelekea nchi yetu kufanya vizuri katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati na hivyo kuihakikishia nchi uhakika wa huduma inayotolewa kwa manufaa ya Taifa letu. Aidha, kamati imeipongeza pia TMA kwa kuongeza ubora na usahihi wa utabiri ikiwemo wa mvua zilizoambatana na Elnino. Pongezi hizo zilipokelewa kwa niaba ya Serikali na Naibu Waziri wa Uchukuzi, Mhe. David M.Kihenzile (MB) ambaye aliongoza uongozi wa Wizara na TMA.

Katika hatua nyingine, Mhe. Kakoso aliagiza uboreshaji wa Chuo cha Taifa cha Hali ya Hewa ufanyike pamoja na maslahi bora ya watumishi. “Tunaiomba Serikali imarisheni Chuo cha Taifa cha Hali ya Hewa ili kiweze kuandaa wataalamu watakaofanya kazi, pili lindeni wafanyakazi wa TMA kwa kuwapatia maslahi mazuri, msipofanya hivyo Serikali itakuwa inasomesha vijana wengi na baadaye wote wanaondoka kwasababu hawalipwi vizuri”. Alisema Mhe. Kakoso.

Awali, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la KImataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt.Ladislaus Chang’a aliishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kutenga fedha zinazowezesha TMA kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo kwa ajili ya kuboresha huduma za hali ya hewa nchini.

 

“Rada hii imesaidia kwa kiasi kikubwa kubaini na kufuatilia mwenendo wa hali ya hewa, vimbunga ziwani,hali mbaya ya hewa,upepo mkali na kutoa tahadhari kwa wananchi hususani watumiaji wa ziwa Viktoria na kuboresha taarifa zinazotolewa na kuimairisha tija na usalama kwa watumiaji wengine wa taarifa za hali ya hewa kama sekta ya usafiri wa anga, ulinzi, kilimo,uvuvi na utunzaji wa misitu”. Alieleza Dkt. Changa.

 

Rada ya hali ya hewa iliyopo Mwanza, inauwezo wa kufanya uangazi wa mikoa ya Mwanza, Shinyanga,Kagera, Mara na eneo kubwa la ziwa vicktoria. Vilevile, rada hii ni moja ya uwekezaji mkubwa unaoendelea wa kukamilisha mtandao wa rada saba zenye teknolojia ya kisasa hapa nchini, ambapo rada tano zimeshafungwa katika mikoa ya Dar es Salaam, Mtwara, Mbeya na Kigoma na rada mbili zitakazofungwa Kilimanjaro na Dodoma zikiendelea na mategenezo Marekani.  

Thursday, February 22, 2024

TMA YATOA UTABIRI WA MSIMU WA MVUA ZA MASIKA 2024 KWA MAENEO YANAYOPATA MVUA MARA MBILI KWA MWAKA.

 






Dar es Salaam; Tarehe 22, Februari 2024.

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa rasmi utabiri wa msimu wa mvua za Masika 2024 kwa maeneo yanayopata mvua mara mbili kwa mwaka. Akizungumza wakati wa mkutano na vyombo vya habari katika ukumbi wa Ubungo Plaza, tarehe 22/02/2024, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya hali ya hewa, Dkt. Ladislaus Chang’a alisema maeneo mengi ya nchi yanayopata misimu miwili ya mvua yanatarajiwa kupata mvua za wastani hadi juu ya wastani.

“Mvua za wastani hadi juu ya wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya nchi, Mvua hizi zinatarajiwa kuanza wiki ya nne ya mwezi Februari katika maeneo mengi na kuisha wiki ya tatu na ya nne ya mwezi Mei 2024, Aidha, aliongeza kuwa ongezeko la mvua linatarajiwa katika kipindi cha mwezi Machi 2024.” Alisema Dkt. Chang’a.

Akizungumzia athari zinazoweza kujitokeza, Dkt. Chang’a alisema vipindi vifupi vya mvua kubwa vinaweza kujitokeza hivyo kuweza kusababisha mafuriko, milipuko ya magonjwa pamoja na athari nyingine zitokanazo na mvua nyingi.

Katika hatua nyingine, Dkt. Chang’a alimshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuboresha miundombinu ya uangazi wa hali ya hewa na hivyo kuiwezesha TMA kufikia hatua ya kuongeza usahihi wa utabiri.

Dkt. Chang’a alisisitiza jamii kuendelea kufuatilia taarifa za mara kwa mara zinazotolewa na TMA kwa vile ni za uhakika, huku akibainisha kuwa usahihi wa msimu wa Vuli 2023 ulikuwa asilimia 98.

Kwa taarifa zaidi tembelea; https://www.meteo.go.tz/news/tma-yatoa-utabiri-wa-msimu-wa-mvua-za-masika-2024-kwa-maeneo-yanayopata-mvua-mara-mbili-kwa-mwaka



Wednesday, February 21, 2024

TMA YAWANOA WANAHABARI KUELEKEA MASIKA 2024









Dar es Salaam; Tarehe 21, Februari 2024

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imekutana na wanahabari kutoka vyombo mbalimbali kujadili kuhusu utabiri wa msimu wa Masika (Machi –Mei) 2024, unaotarajiwa kutolewa tarehe 22 Februari 2024. Utabiri huu ni mahususi kwa maeneo yanayopata mvua mara mbili kwa mwaka ambayo ni Dar es Salaam, Pwani, Kaskazini mwa Morogoro, Visiwa vya Unguja na Pemba, Tanga, Kilimanjaro,Arusha, Manyara,Simiyu, Mara, Geita, Mwanza, Shinyanga, Kagera na Kaskazini mwa Kigoma. Mkutano huo ulifanyika katika ukumbi wa Chuo cha Biashara (CBE), Dar es Salaam, Tarehe 21/2/2024.

Akizungumza wakati wa ufunguzi rasmi, Dkt. Ladislaus Chang’a, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, alisema “Mkutano huu ni mwendelezo wa sehemu ya ushirikishwaji wa wanahabari katika kuandaa taarifa zinazolenga kuchochea matumizi sahihi ya huduma za hali ya hewa”. 

Aidha aliendelea kusisitiza kuwa, uzingatiaji wa taarifa  za hali ya hewa, hususan tahadhari za matukio ya hali mbaya ya hewa ni muhimu sana katika kuokoa maisha ya watu na mali zao na katika kuongeza tija na ufanisikatika kupanga na kutekeleza mipango ya kiuchumi na kijamii, ikiwemo katika sekta za kilimo, ujenzi, Afya, Maji, Ulinzi, Usafiri (Anga, Maji na Nchi Kavu), Madini, Utalii, shughuli za Bandari nk..

Dkt. Chang’a alisema kwa kuzingatia umuhimu huo wa huduma za hali ya hewa nchini, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kipindi chake imeendelea na jitihada za kuimarisha huduma za hali ya hewa nchini ikiwemo uwekezaji mkubwa katika miundo mbinu ya uangazi, uchakati wa data na utabiri, ikiwa ni utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi Ibara ya 59J. Hivyo, aliishukuru Serikali na wadau wa maendeleo kwa kuendelea na uwekezaji katika miundombinu ya hali ya hewa hapa nchini kupitia mpango wa bajeti na programu mbalimbali za maendeleo, hali inayochangia Mamlaka kuendelea kuboresha huduma zake. 

Naye Mwakilishi wa washiriki kutoka gazeti la Majira, Bi. Penina Malundo,  aliishukuru TMA kwa ushirikiano wanaoendelea kutoa kwa waandishi wa habari  katika kuhakikisha wanaandika habari za hali ya hewa kwa ufanisi na uweledi ili wananchi waweze kuelewa. 

“Utoaji wa mafunzo kwa waandishi wa habari umeweza kuongeza tija kwa wananchi kufuatilia taarifa hizo katika kufanya shughuli zao hususan za kijamii”. Alisema Bi. Penina.

Katika mkutano huu, wanahabari walipata fursa ya kuona utabiri wa hali ya hewa katika kipindi cha mwezi Machi hadi Mei, 2024 na kutoa michango yao juu ya namna sahihi ya usambazaji wa taarifa katika kipindi chote cha msimu.

Saturday, January 20, 2024

VIPINDI VYA MVUA KUBWA KATIKA BAADHI YA MAENEO NCHINI


 ​Dar es Salaam, 20 Januari, 2024:

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) inapenda kutoa taarifa ya vipindi vya mvua kubwa vilivyojitokeza katika baadhi ya maeneo nchini.

Mvua zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali hapa nchini zimepelekea uwepo wa athari katika baadhi ya maeneo. Mnamo usiku wa tarehe 19 kuamkia tarehe 20 Januari, 2024 vimejitokeza vipindi vya mvua kubwa zilizoambata na upepo mkali katika baadhi ya maeneo nchini na kusababisha athari ikiwemo mafuriko, uharibifu wa mali na miundombinu. Maeneo yaliyokumbwa na mvua hizo ni pamoja na Mikoa ya Tanga, Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Lindi, Mtwara, Arusha, Kilimanjaro na Manyara pamoja na Visiwa vya Unguja na Pemba. Hadi kufikia saa 3 asubuhi ya leo (20 Januari, 2024) kituo cha Zanzibar kiliripoti kiasi cha milimita 85.2 za mvua kwa saa 24 ikifuatiwa na kituo cha Kibaha milimita 84.8 na Dar es Salaam milimita 54.6.

Uwepo wa mvua hizo unasababishwa na kuimarika kwa mifumo ya hali ya hewa inayosababisha mvua nchini ikiwemo hali ya El-NiƱo kama ilivyoelezwa hapo awali. Aidha, Ukanda Mvua pamoja na kuimarika kwa migandamizo midogo ya hewa iliyopo mashariki mwa kisiwa cha Madagascar imepelekea pia kuwepo na vipindi vya mvua kubwa. Migandamizo hiyo midogo ya hewa inapelekea kuvuta upepo wenye unyevunyevu kutoka magharibi (Misitu ya Kongo) kuelekea baadhi ya maeneo ya nchini. Aidha, katika taarifa za mwelekeo wa mvua za Vuli, 2023 iliyotolewa tarehe 24 Augusti, 2023 na Mvua za Msimu 2023/2024 iliyotolewa tarehe 31 Oktoba, 2023 zilionesha uwepo wa vipindi vya mvua za nje ya msimu katika kipindi cha miezi ya Januari na Februari, 2024 hususan katika maeneo yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka.

Uchambuzi wa mifumo ya hali ya hewa bado unaendelea kuonesha uwepo wa hali hiyo ya vipindi vya mvua vya nje ya msimu. Mamlaka inaendelea kufuatilia mienendo ya hali ya hewa nchini na kutoa mrejeo pale itakapobidi. Kwa taarifa hii wananchi wanashauriwa kuendelea kuzingatia taarifa na tahadhari za hali mbaya ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania sambamba na kutafuta, kupata na kufuata ushauri wa wataalam katika sekta husika ili kupunguza athari zinazotokana na hali mbaya ya hewa.

Wednesday, January 17, 2024

Chair) katika Mkutano wa 60 wa IPCC (IPCC-60)



Mojawapo ya majukumu ya TMA ni kuwakilisha Tanzania Kikanda na Kimataifa katika Masuala ya Hali ya Hewa. Pichani ni Dkt. Ladislaus Chang'a, Kaimu Mkurugenzi Mkuu (TMA) na Makamu wa Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi -IPCC (IPCC-Vice Chair) katika Mkutano wa 60 wa IPCC (IPCC-60), Instanbul, Uturuki, tarehe 16-19 Januari 2024.

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...